Designer Hebron Malele More information *Phone number 0659-994437*: hebronjohana@yahoo.com!!  NICE FOR ALL :

Saturday, 6 June 2015

#HABARI:Wabunge wamshukia Prof Maghembe.


Dodoma. Wabunge wamembana Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe wakimtuhumu kuandaa taarifa za uongo, ufisadi na ubabaishaji kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji kwa mwaka 2014/15, kuziwasilisha bungeni wakati hali halisi ikionyesha kuwa maeneo mengi nchini wananchi hawapati maji.
Bila kujali itikadi zao za kisiasa, wamesema hata hotuba ya bajeti ya wizara hiyo ya mwaka 2015/16, haina jipya huku Mbunge wa Nyamagana (Chadema), Ezekia Wenje akiomba muongozo kwa Spika ili waziri huyo afukuzwe bungeni akarekebishe takwimu zake.
Akichangia mjadala wa Bajeti ya wizara hiyo ya mwaka 2015/16 ambayo ilipitishwa jana jioni, Wenje alisema hotuba ya waziri huyo imejaa ubabaishaji, uongo na ufisadi, “Mheshimiwa Spika naona lingekuwa jambo jema kama waziri (Maghembe) afukuzwe humu ndani ili aende kuandaa takwimu sahihi za wizara yake. Amelidanganya Bunge kwa kutoa takwimu za uongo juu ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Jambo hili halikubaliki katika dhana ya utawala bora.”
“Ni jambo la ajabu sana na ukiona uongo unatamkwa wazi humu ndani ujue kuna hela zimepigwa. Inakuwaje unasema imetekelezwa miradi 53 wakati iliyotekelezwa ni miwili tu,” alihoji Wenje.
Mbunge wa Nkasi Kaskazini (CCM), Ally Keissy alisema: “Waziri amepokea takwimu za uongo kabisa hizi ambazo hata utafiti hazijafanyiwa. Hapa ni wazi kuwa fedha za wizara na halmashauri zimeliwa.” Keissy alisema Sh1 bilioni zilizoahidiwa na Rais kuwa zitakwenda katika jimbo hilo, zimefika Sh500 milioni tu na kati ya hizo Sh8 milioni zimeshatafunwa na watumishi wa wizara hiyo.
“Nimekuwa nikitoa taarifa kwa Waziri Maghembe juu ya wizi mkubwa wa fedha katika miradi ya maji katika wilaya ya Nkasi, hasa eneo la Namanyere, Kirando, King’ombe na maeneo mengine lakini cha ajabu Waziri anakuja hapa na takwimu kuwa maji yanatoka,”alisema kwa kufoka. Naye Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema), David Silinde alitoa mpya baada ya kusema kuwa anatamani kumcharaza bakora Profesa Maghembe kutokana na kutoa taarifa za uongo bungeni kila mara.
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Azza Hillal alisema, “Hotuba ya waziri inasema vituo vya maji vinavyofanyakazi katika kijiji cha Kagongwa ni 22 lakini ukweli ni kwamba vituo vilivyopo ni vinane tu.”
Akizungumzia hayo, Mbunge wa Rungwe Magharibi (CCM), Profesa David Mwakyusa alimtaka Profesa Maghembe kutoona aibu kuweka kipaumbele katika kutekeleza miradi ya zamani badala ya kuomba mipya ambayo haitekelezeki.
Kauli ya Kamati
Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji imesema Serikali haina nia ya dhati ya kupunguza tatizo la maji nchini kutokana na kutoa asilimia 26 tu ya fedha za maendeleo za Bajeti ya Wizara ya Maji mwaka 2014/15. Akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo, mwenyekiti wake Profesa Peter Msolla alisema wizara hiyo iliidhinishiwa Sh488.8bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo, lakini mpaka kufikia Machi mwaka huu wizara hiyo ilikuwa imepokea Sh129.3bilioni.
Kambi ya Upinzani
Akiwasilisha taarifa ya kambi ya upinzani ya Wizara ya Maji kwa niaba ya waziri kivuli wa wizara hiyo, Magdalena Sakaya, mbunge wa Ole (CUF), Rajab Mbarouk alisema sekta ya maji inakabiliwa na upungufu wa watumishi 6,901. Takwimu za wizara zinaonyesha wataalam wanaohitajika ni 8,749 lakini waliopo ni 1,848,” alisema.

No comments:

Post a Comment